Iran na Marekani zalaumiana huku vikwazo dhidi ya Iran vikitarajiwa kuanza kutekelezwa.
Vikwazo ambavyo Marekani imeviwekea Iran vinatarajiwa kuanza kutekelezwa leo, huku viongozi wa Iran na Marekani wakilaumiana. Baada ya Trump kusema milango yake iko wazi kwa mazungumzo, lakini akaiambia Iran kubadili kile alichokitaja kuwa “tabia ya udhoofishaji” la sivyo itengwe zaidi kiuchumi, rais wa Iran Hassan Rouhani ameilaumu Marekani kwa kuendeleza kile alichokitaja kuwa “vita vya kisaikolojia”.
Kauli hizo zimejiri wakati vikwazo dhidi ya Iran vikitarajiwa kuanza kutekelezwa leo. Awamu ya kwanza ya vikwazo hivyo vinalenga kuizuia nchi hiyo ya Kiislamu kutopata dola za Marekani na pia vinalenga viwanda muhimu vikiwemo vya magari na mazulia.
Iran ilikataa pendekezo la Trump la kufanya mazungumzo kuhusu mkataba mpya wa nyuklia, baada ya Rais Donald Trump kuiondoa Marekani kwenye mkataba huo wa mwaka 2015 kuhusu silaha za nyuklia.